May 02, 2014

Gari la Mbowe lakamatwa nchini Kenya likihisiwa kuhusika na UGAIDI nchini humo.....Gari hilo lilikuwa na namba mbili, STK na KUB...Polisi Kenya yamsubiri Mbowe kwa mahojiano



GARI la Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, limekamatwa na kuendelea kushikiliwa mjini Mombasa nchini Kenya, kutokana na kuwa na namba mbili.

Taarifa za  jana  kutoka Kenya  zilieleza kuwa polisi nchini Kenya walipata taarifa za kuwepo kwa gari hilo na watu ambao walionekana kutokuwa na kazi maalumu.
Baada ya kupata taarifa hizo, Polisi hao walio katika msako wa wageni na magari yanayotiliwa shaka kuhusika katika uhalifu na ugaidi, walianza kulifuatilia na kubaini wahusika wa gari hilo.
Ufuatiliaji huo kwa mujibu wa taarifa hizo, ulibaini wahusika wa gari hilo walipofika Mombasa kutokea Tanzania, hawakuonekana kupokewa na mwenyeji yeyote, hali inayomaanisha wenyewe ni wenyeji wa mji huo.
Taarifa za Polisi zilibainisha kuwa uchunguzi wao ulibaini kuwa gari hilo liliwabeba Mbowe, Mbunge wa Mwanza Mjini, Ezekiah Wenje na dereva Ibrahim Nguzo.
Polisi hao inadaiwa walitilia shaka gari hilo kutokana na kuwa na namba za usajili STK 8146, ambazo zilipandishiwa juu ya nambari halisi za gari hilo ambazo ni KUB.
Uchunguzi wa Polisi hao ulibaini kuwa Mbowe na Wenje waliwasili Mombasa, Kenya kwa gari wakitokea Tanzania kupitia mpaka wa Horohoro/Lungalunga na kwenda moja kwa moja hotelini.
Mashaka kwa Polisi hao yaliongezeka baada ya Mbowe na Wenje Aprili 26 mwaka huu kusafiri kwenda Nairobi kwa ndege, na kumwacha dereva pamoja na gari hotelini.
Kutokana na hali hiyo, Jumatatu wiki hii saa 5.00 asubuhi askari Polisi wa Mombasa walimkamata Ibrahim pamoja na gari hilo, baada ya kuonekana amekaa hotelini muda mrefu bila ya shughuli zozote.
“Hapo ndipo alipotoa habari kwamba alikuwa akiwasubiri wakubwa zake ambao walikwenda Nairobi tangu Aprili 26 na hawakuwa wamerejea,” ilieleza taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Ibrahim alipoulizwa kwa nini gari lilikuwa na nambari za kupandishiwa, alijibu huo ulikuwa ni uamuzi wa bosi wake Mbowe.
Polisi hao waliamua kukamata gari hilo na kulipeleka katika kituo cha Polisi cha Kati kwa mahojiano zaidi na baada ya mahojiano, aliachiliwa Ibrahim huru lakini gari limeendelea kuzuiliwa kituoni hadi Mbowe na Wenje watakapofika kwa ajili ya kuhojiwa.
Gazeti hili lilimtafuta msemaji wa Chadema, Tumaini Makene, ambaye aliomba muda kupata taarifa halisi za tukio hilo na baadaye alituma ujumbe mfupi wa maneno ambao hakukanusha wala kukubali kutokea kwa tukio hilo.
“Suala hilo ni la kiutawala napendekeza utafute uongozi wa Bunge…mtafute Katibu wa Bunge (Dk Thomas Kashililah), bila shaka ataweza kukueleza juu ya safari ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni na mengine yote ya kiutawala unayotaka kupata majibu yake,” alieleza Makene.

  
>>Habari leo

SHARE THIS POST TO SOCIAL MEDIA BELOW: