April 09, 2014

YANGA..AZAM UKILALA UMELIWA

YANGA na Azam FC leo zinaendelea na mchuano wao mkali wa kuwania ubingwa wa soka wa Tanzania Bara wakati zitakaposhuka dimbani katika v... thumbnail 1 summary

YANGA na Azam FC leo zinaendelea na mchuano wao mkali wa kuwania ubingwa wa soka wa Tanzania Bara wakati zitakaposhuka dimbani katika viwanja viwili kuwania pointi tatu muhimu.


Vinara Azam FC watasafiri hadi Mlandizi mkoani Pwani kwenye Uwanja wa Mabatini kuikabili Ruvu Shooting Stars ya huko wakati wanaoshika nafasi ya pili, mabingwa watetezi, Yanga watakuwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuwakabili Kagera Sugar ya Missenyi mkoani Kagera.

Azam FC inayosaka ubingwa wa Tanzania Bara kwa mara ya kwanza, iko kileleni ikiwa na pointi 53 baada ya timu zote kushuka dimbani mara 23, wakati Yanga ni ya pili kwa kuwa na pointi 49.

Zikishinda mechi zao tatu zilizobaki zikiwamo za leo, Azam FC itafikisha pointi 62 na Yanga itafikisha pointi 58, hivyo vijana hao wa Chamazi, kutawazwa bingwa kwa mara ya kwanza.

Mbali ya mechi ya leo, Azam FC itashuka dimbani Aprili 13, kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya kuikabili Mbeya City na kumalizia ligi Aprili 19, mwaka huu kwa kuivaa JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Azam Complex.

Yanga mbali ya kuivaa Kagera Sugar leo, itakuwa mwenyeji wa JKT Oljoro, Aprili 13, mwaka huu jijini Arusha, kabla ya kumalizia na watani wao wa jadi, Simba, Aprili 19 kwenye Uwanja wa Taifa.

Kwa hiyo, kwa hesabu hizo, hakuna timu inayohitaji kulala kwani endapo mojawapo italala, uwezekano wa mwenzake kuwa bingwa ni mkubwa na hasa kwa upande wa Yanga ambayo ikiteleza tu, Azam bingwa.


KWA HABARI MOTOMOTO BONYEZA HAPA KU-LIKE PAGE YETU FACEBOOK NA WHATSAPP
Ni kwa msingi huo, kila mechi kwa kila timu ni fainali kwao ndio maana macho na masikio ya mashabiki wa soka leo yataelekezwa Mabatini, Pwani na Taifa, Dar es Salaam kufahamu nini kitatokea.

Katika kujiimarisha na mechi ya leo, wachezaji wa kimataifa wa Yanga, Haruna Niyonzima na Emmanuel Okwi, watakuwa ni miongoni mwa wachezaji watakaoivaa Kagera Sugar.

Wachezaji hao pamoja na David Luhende na Athuman Idd hawakuwemo kikosi kilichoivaa JKT Ruvu mwishoni mwa wiki iliyopita wakidaiwa kuwa ni wagonjwa.

Kwa mujibu wa tovuti ya Yanga, wachezaji hao wanaendelea vizuri na kwamba walijiunga kwenye mazoezi toka juzi.

“Wachezaji wote wanaendelea vizuri na mashabiki wategemee kuwaona uwanjani leo,” alisema Kocha Mkuu wa Yanga, Hans van der Pluijm.


Pluijm alisema vijana wake 20 walioingia kambini wote wapo kwenye hali nzuri, kiafya, kifikra na morali ya kusaka pointi tatu kwani wanahitaji kutetea ubingwa tena kwa msimu wa pili mfululizo.

Katika mchezo wa awali uliozikutanisha Kagera Sugar na Yanga kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, Yanga ilishinda mabao 2-1, wafungaji wakiwa ni Mrisho Ngasa na Hamisi Kiiza. Ligi hiyo itaingia raundi ya 25, Aprili 12 na 13 mwaka huu ambapo timu zote 14 zitakuwa viwanjani.

Aprili 12 mwaka huu itakuwa Mtibwa Sugar dhidi ya Ruvu Shooting (Manungu, Morogoro), Coastal Union itaikabili JKT Ruvu (Mkwakwani, Tanga), na Tanzania Prisons itakuwa mwenyeji wa Rhino Rangers (Sokoine, Mbeya).

Aprili 13, mwaka huu ni Mgambo Shooting itacheza na Kagera Sugar (Mkwakwani, Tanga), Simba itakuwa mwenyeji wa Ashanti United (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam), Mbeya City itaialika Azam (Sokoine, Mbeya) na Oljoro itawakaribisha Yanga (Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha).

SHARE THIS POST TO SOCIAL MEDIA BELOW: